Monday, November 26, 2012

Hatuongezi muda kuingia digitali

Na Beatrice Shayo

Mamlaka ya Mawasiliano nchini (TCRA), imesema haitaongeza muda wa kujiunga na mfumo wa digitali na ifikapo Desemba 31, mwaka huu itakuwa mwisho wa kutumia teknolojia ya zamani ya analogia.
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Meneja wa Mawasiliano TCRA, Innocent Mungy, katika semina ya wadau wa Manispaa ya Temeke juu ya haki na wajibu wa watumiaji wa huduma za mawasiliano, alisema wananchi wanatakiwa kuzingatia muda uliowekwa.
Alisema ikifika Desemba 31 mwaka huu, kama kutakuwa na mtu ambaye hajajiunga na mfumo wa digitali hataweza kuona matangazo wala kurusha, hivyo ni muhimu watu kutafuta ving'amuzi mapema.
Mungy alisema mtu yeyote ambaye atanunua king'amuzi hataingia gharama za kulipia kwa mwezi na kwamba atakuwa akiona matangazo ya televisheni za ndani bure lakini akitaka kuona matangazo ya vituo vya kimataifa kama CNN, BBC na KBC atalipia.
Hata hivyo, alisema baadhi ya wananchi hawajawa na uelewa kuhusu mfumo huo mpya na kudhani wanatakiwa kununua televisheni mpya.
Alisema kinachotakiwa ni kununua king'amuzi kutoka kampuni za Star Times au Agape lakini televisheni zitakazotumika ni zilezile.
Alisema tayari kampuni hizo zimeshajulishwa kuwa zitatakiwa kuonyesha vipindi vya nchini bure.
Akizungumzia suala la kuwepo kwa simu feki nchini, Mungy alisema wanajipanga kwa kushirikiana na mamlaka nyingine katika kuzuia tatizo hilo.
Alisema kwa sasa wanachokifanya ni kutoa mafunzo kwa wananchi hasa katika maeneo ya vijijini kuacha kununua simu feki.
Mungy alisema endapo wakizuia simu hizo zisitumike kwa sasa wananchi wengi wataathirika zaidi katika zoezi hilo, hivyo wanalifanyia kazi na watatoa taarifa ya kusitishwa kwa utumiaji wa simu feki ili watu wasiathirike.
Kwa upande wake mjumbe ambaye alikuwa akiwakilisha chama cha wazee, Bregadia Jenerali Mstaafu, Francis Mbeuna, alisema mafunzo ambayo yanatolewa na TCRA yatawasaidia kujua haki zao ya msingi.
Alisema anaunga mkono suala la kuingia kwenye mfumo wa digitali na kwamba inaonyesha kuwa Tanzania inakwenda na wakati kama nchi zingine.
Naye Diwani wa Viti maalum Temeke, Mariamu Mtevu, alisema kuwa serikali iangalie namna ya kuwapunguzia ving'amuzi hivyo ili kila mmoja aweze kuvinunua kwani gharama ni kubwa.
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

No comments: