Monday, November 26, 2012

Dk Slaa azushiwa kifo

Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Wilbroad Slaa
Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Wilbroad Slaa , jana amezushiwa kufariki dunia, kufuatia ajali mbaya ya gari.
Habari zilizosambaa kupitia simu za mikononi na watu mbalimbali waliokuwa wakipiga simu chumba cha habari, zilidai kuwa Dk Slaa ambaye alikuwa safarini katika ziara yake ya kikazi amepata ajali ya gari maeneo ya Dodoma na Morogoro na kufariki dunia.
Habari hizo hata hivyo zilikanushwa na Dk. Slaa mwenyewe baada ya kupigiwa simu yake ya mkononi.
Akiongea na mwandishi wa habari hizi, Dk. Slaa alisema anamshukuru Mungu kuwa hao wanaomzushia kifo wanazidi kumuongezea maisha na kumpa nguvu na kuendelea na kazi zake.
“Hizo ni propaganda za watu wasionitakia mema, hivi ninavyoongea na wewe niko katika kijiji cha Nkwenda, Wilaya mpya ya Kyelwa, huku Bukoba ndio nimetoka kuteremka kwenye jukwaa kuongea na wananchi,” alisema Dk. Slaa na kuongeza “Mimi ni mzima kabisa na nikitoka hapa nakwenda kwenye mkutano mwingine.”
Alisema hiyo si mara ya kwanza yeye kuzushiwa kifo, lakini anamshukuru Mungu kuwa wabaya wake wanavyozidi kumzushia habari mbaya wanaendelea kumuongezea siku za kuishi.
Dk. Slaa alisema anaamini watu wanaozusha habari hizo wana nia mbaya ya kumdhoofisha kisiasa lakini kwa uwezo wa Mungu ataendelea kupigania haki za wananchi.
Akidhihirisha kuwa yu mzima wa afya, Dk. Slaa alisema anaendelea na kazi zake za chama na kwamba akitoka kwenye wilaya hiyo mpya anaekelekea kwenye wilaya nyingine kwa kazi yake ya kueneza sera ya chama chake.
Dk Slaa pia alikiri kupokea simu kutoka kwa watu mbalimbali waliokuwa wakiulizia hali yake baada ya kuenea kwa habari za kuzushiwa kifo.
“Nashukuru kuwa watu wananipenda maana baada tu ya kupata habari hizo walikuwa wakinitafuta kwenye simu yangu kujua ukweli,” alisema.
Hii ni mara ya pili kwa Dk. Slaa kuzushiwa kifo, mara ya kwanza aliwahi kuzushiwa kuanguka bafuni na kupoteza maisha.
Tabia hii ya watu hasa maarufu kuzushiwa taarifa za vifo imekuwa ni mtindo kwa baadhi ya watu na kusababisha usumbufu mkubwa kwa familia, ndugu na jamaa za watu hao.
Watu wengine wanaolengwa na habari hizo za kizushi ni pamoja na wasanii wenye majina makubwa na hivi karibuni msanii wa siku nyingi maarufu kama Bi Kidude aliwahi kuzushiwa kifo.
SOURCE: NIPASHE JUMAPILI

No comments: