Friday, November 23, 2012

Rais Museveni aandaa mazungumzo na M23

Waasi wa M23
Waasi wa M23
Waasi nchini Jamuhuri ya Kidemokrasi ay Congo, wamepuuzilia mbali wito kutoka kwa viongozi wa kimataifa wa kusitisha mapigano na pia kuondoka kutoka mji wa Goma Mashariki mwa nchi hiyo.
Msemaji wa kundi hilo la waasi wa M23, amesema wapiganaji wao wataendelea na mapigano hayo hadi pale serikali ya rais Joseph Kabila itakapokubali kutekeleza masharti yao.
Awali rais wa Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Congo, alisema yuko tayari kuchunguza malalamishi ya wapiganaji wa waasi ambao wameuteka mji wa Goma, Mashariki mwa nchi hiyo.
Akiongea baada ya mazungumzo yaliyofanyika nchini Uganda na Kuhudhuriwa na rais wa Rwanda, Paul Kagame, Rais Joseph Kabila amesema anatathmini uwezekano wa kuanzisha mazungumzo na waasi hao wa M23.
Mwenyekiti na mwenyeji wa Mazungumzo hayo, rais wa Uganda Yoweri Museveni, rais Kabila na Kagame kwa kauili moja walitoa wito wa kusitishwa kwa mapigano hayo na pia kutoa amri kwa waasi hao kuondoka Goma mara moja.
Wapiganji hao wa waasi wametishia kuendeleza mapigano hayo hadi mji mkuu wa nchi hiyo Kinshasa.

Mazungumzo ya amani

Wanajeshi wa Serikali ya Congo
Wanajeshi wa Serikali ya Congo
Wakati huo huo, ripoti zinasema kuwa rais wa M23 yuko njiani kuelekea mjini Kampala kwa mazungumzo na rais YowerI Museni.
Rais Museveni, ameitisha kikao na viongozi wa waasi hao ili kujadili harakati za kumaliza mzozo huo Mashariki mwa Congo, na yametokea siku moja tu, baada ya rais huyo wa Uganda kufanya mashauriano mengine na rais Kabila na mwenzake kutoka Rwanda Paul Kagame.
Hapo jana, wapiganaji hao wa M23 waliuteka mji wa Sake, ulioko takriban kilomita 27, kutoka Goma.
Ripoti zinasema wapiganaji hao sasa wanajiandaa kuelekea eneo la Kusini hadi Bukavu, takriban kilomita 230 kutoka Goma.
Kamanda mmoja wa waasi hao, aliliambia umati wa watu waliokusanyika katika uwanja wa michezo mjini Goma, kuwa safari yao ya kukomba taifa hilo imeanza.
Lakini mwandishi wa BBC mjini Goma, anasema haijabainika wazi ikiwa wapiganaji hao wa waasi wana uwezo wa kutekeleza vitisho vyao.
Kundi hilo la M23 liliundwa mwezi April mwaka huu baada ya wanajeshi kadhaa kuasi.
Wapiganaji hao wa waasi wanasema hawakupewa nyadhifa za kijeshi walizohaidiwa baada ya kusainiwa kwa mkataba wa amani mwaka wa 2009.
Vitendo vya wapiganaji hao wa M23, vimezua wasi wasi wa kuzuka upya kwa mapigano nchini Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Congo, ambako takriban watu milioni tano waliauawa kufuatia mapigano yaliyoanza mwaka wa 1997 na kumalizika mwaka wa 2003.

No comments: