Thursday, November 22, 2012

Kenya itawapa nafasi wanawake kuongoza?


James Mbugua
Mwanamke raia wa Kenya
Uchaguzi mkuu ujao nchini Kenya utashuhudia mabadiliko mengi sio tu kwa nyadhifa mbali mbali zitakazo waniwa lakini pia kwa idadi ya wanawake wanao paswa kuchaguliwa.
Kwa mujibu wa katiba mpya ya Kenya, jinsia moja haiwezi kushikilia zaidi ya thuluthi mbili ya viti vitakavyo gombewa. Hii ni maana kwamba lazima wakenya wachagua thuluthi moja ya jinsia moja iwe wanaume au wanawake ili kutimiza sheria hiyo mpya, hasa kwa bunge za kitaifa na za kaunti.
Kwa sababu wanaume ndio wengi katika bunge la sasa, itakuwa kibarua kigumu kutimiza sheria hiyo na kuhakikisha wanawake wanashikilia thuluthi moja ya viti katika bunge la kitaifa na zile za kaunti.
Kwa sasa Kenya ina wabunge wanawake 22 kati ya wabunge 222 .
Hata hivyo katiba imetenga viti 47 vya wanawake pekee. Lakini licha ya kutengewa viti hivi 47, kuna hofu kwamba idadi ya wanawake watakao chaguliwa haitaweza kufikia 117, ili kutimiza maudhui hio ya sheria mpya.
Iwapo sheria hii ya uwakilishi wa wanawake katika uongozi haitatimizwa itamaanisha kwamba Kenya huenda ikashuhudia mzozo wa kikatiba.
Kwa sasa kuna kesi kuitaka mahakama itafsiri sheria hiyo. Je ina maana kwamba iwapo bunge litakalo chaguliwa litazidisha thuluthi mbili ya jinsia moja, kutakuwa na mzozo wa kikatiba?
Basi usikose kusikiliza kipindi maalum cha Sema Kenya, ambapo tutajadili swala hili.
Aidha, utaweza pia kusikiliza changamoto zinazowakabili wanawake nchini Kenya katika kupata nyadhifa hizi za uongozi.
Wakenya 100 wa tabaka mbalimbali watalijadili suala hili la kushirikisha wanawake katika uongozi .
Kujadili swala hili tumewaalika wataalam mbali mbali wa maswala ya jinsia na katiba wakiwemo Winnie Lichuma, kamishna wa tume ya jinsia na usawa nchini Kenya, Mbunge wa kuteuliwa, Sophia Abdi Noor, Bobby Mkangi- ambaye alihusika katika kutunga sheria mpya ya Kenya na mtalaam wa maswala ya jinsia profesa Nyokabi Kamau ambaye ni mhadhiri wa chuo kikuu nchini Kenya.
Basi usikose kujiunga na mjadala huu wa kitaifa Jumapili hii, tarehe 11 Novemba. Makala haya hupeperushwa kupitia redio ya BBC saa saba mchana na kupitia runinga ya KTN nchini Kenya saa kumi na mbili jioni.

No comments: