Friday, November 23, 2012

Dk. Mwakyembe awageukia watendaji wa wizara yake

Na Dege Maso

Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe

Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe, ameendelea kuwa mwiba mkali kwa kupiga marufuku usafiri wa daraja la kwanza kwa watendaji wakuu wanaokwenda nje ya nchi na kutangaza kuchukua hatua kali kwa watakaokiuka agizo hilo.
Akizungumza na waandishi wa habari jana Jijini hapa, Dk. Mwakyembe alisema agizo hilo linawahusu watendaji wakuu wa mashirika yote yaliyopo ndani ya Wizara ya Uchukuzi.
Alisema lengo la marufuku kwa watendaji hao kutumia usafiri wa daraja la kwanza ni kuzuia ufisadi na matumizi mabaya ya kodi za wananchi ambao ni walalahoi.
“Mimi Waziri natumia usafiri wa daraja la pili kwenda nje ya nchi, lakini watendaji wakuu wanatumia daraja la kwanza…jambo hili halipendezi na wenzetu wa nchi nyingine wanatushangaa,” alisema.
Dk. Mwakyembe alionya kwamba yeyote atakayebainika kwenda kinyume na agizo hilo atachukuliwa hatua ikiwemo kukatwa fedha za usafiri katika mafao yake.
Waziri Mwakyembe yupo Jijini hapa kwa ajili ya kukutana na bodi mpya ya wakurugenzi na kupanga mikakati ya utendaji.
Pia alitangaza mkakati wa kuzuia usajiri wa vyombo vya majini vyenye umri wa zaidi ya miaka 15 kwa lengo la kudhibiti ajali za majini.
Alisema mkakati mwingine ni kuhakikisha kila chombo chenye sifa ya kutoa huduma za usafiri wa majini kinakuwa na vifaa vya kutosha vya uokoaji na kupakia kwa mujibu wa uwezo wa chombo husika na kwamba kila abiria ataruhusiwa kupanda ndani ya chombo hicho kwa kutumia kitambulisho cha uraia na si vinginevyo.
Kwa upande mwingine, Dk. Mwakyembe alisema serikali ya Tanzania pamoja na ya Denmark imeanza mchakato wa kupata meli mpya kubwa ambayo itakuwa suluhu la tatizo la usafiri wa majini pamoja na kuangalia uwezekano wa kusimamisha meli za zamani ikiwemo ya MV. Liemba ambayo inakaribia takriban miaka 100 sasa.  
CHANZO: NIPASHE

No comments: