Friday, May 17, 2013

Je ,Syria inatumia sumu kuwaua raia wake?


Kanda inayoonyesha hali ya mapigano nchini Syria

BBC imeonyeshwa,ushahidi unaothibitisha kufanyika kwa mashambulizi ya silaha za kemikali dhidi ya raia mwezi jana nchini Syria.
Mwandishi wa BBC, aliyezuru mji wa Kaskazini wa Saraqeb, aliambiwa na walioshuhudia mashambulizi hayo kuwa ndege za helikopta za serikali zilirusha ardhini vifaa viwili vilivyokuwa na gesi ya sumu.
Serikali hata hivyo imekanusha madai hayo, kuwa imetumia kemikali zenye sumu dhidi ya raia.
Marekani imeonya kuwa tukio kama hilo litailazimisha nchi hiyo kuingilia mzozo huo kama njia ya kutuliza hali.
Hata hivyo, rais Barack Obama, amesema kuwa ushahidi wa sasa kuwa serikali ilitumia gesi ya sumu dhidi ya raia , hautoshi kwa nchi hiyo kuingilia kati.
Mwezi Aprili tarehe 29, mji wa Saraqeb, ulioko Kusini Magharibi mwa Allepo, ulishambuliwa kwa mabomu na wanajeshi wa serikali.
Madaktari katika moja ya vituo vya matibabu aliambia mwandishi wa BBC kuwa wamewalaza wagonjwa wanane wanaokabiliwa na matatizo ya kupumua. Baadhi walikuwa wanatapika na wengine macho yao wakionekana kuingia ndani. Mmoja wa waathiriwa Maryam Khatib alifariki baadaye.
Kanda kadhaa za video, zilizokabidhiwa kwa BBC zinaonekana kuthibitisha madai haya, lakini ni vigumu kuyathibitisha.
Mwanawe Bi Khatib aliyeenda kumwokoa mamake , naye pia alijeruhiwa katika shambulizi hilo.

Je Syria inatumia silaha za kemikali?

"ilikuwa harufu mbaya yenye kumsakama mtu. Hungeweza kupumua. Ungehisi kama unafariki.Hata haungeweza kuona. Mwenyewe sikuweza kuona chochote kwa siku tatu au nne,'' alisema Khatib
Daktari aliyekuwa anamtibu Bi Khatib, alisema kuwa dalili alizokuwa nazo ni kama za kuathirika kutokana na sumu, lakini uchunguzi unafanyika.
Moja ya vifaa ambavyo inasemekana vilikuwa na gesi hiyo , kilianguka viungani mwa mji wa Saraqeb, huku waliokishuhudia wakisema kuwa kilikuwa kama kisanduku kidogo cha simiti chenye shimo ambalo moshi ulikuwa unapitia.
Kanda nyingine ya Video, inaonyesha kukiwa na unga unga mweupe katika sehemu ambapo sanduku hiyo iliangushwa.
BBC imeambiwa kuwa Uchunguzi zaidi kuweza kubaini ikiwa ni silaha za sumu zinazotumika nchini syria utafanyika nchini Uingereza, Ufaransa , Uturuki na Marekani.

No comments: