Wednesday, May 22, 2013

Mapigano yaendelea kwa siku ya pili Goma

Mamia wanatoroka maeneo ya vita Goma kukimbilia usalama wao

Makabiliano kati ya jeshi na waasi wa kundi la M23 Mashariki mwa Congo yameendelea kwa siku ya pili.
Pande hizo mbili, zilifyatuliana risasi mjini Goma huku kila upande ukituhumu mwingine kwa kuanzisha uchokozi na kuchochea mapigano.
Mapigano yalianza Jumatatu na kumaliza makubaliano ya miezi sita ya kusitisha vita kati ya wanajeshi wa serikali na waasi wa kundi la M-23 , ambao waliwahi kuteka mji wa Goma mwaka jana ingawa kwa muda mfupi.
Mtaalamu wa maswala ya kijeshi amesema kuwa waasi wa M23 wanatumia makombora na magari ya kivita ambayo waliyapokonya wananajeshi Novemba mwaka jana.
Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki Moon anayetarajiwa kuzuru Goma wiki hii alisema ataharakisha mpango wa kupelekwa kwa wanajeshi wa Umoja wa mataifa katika eneo hilo kujaribu kusitisha uasi .
Kikosi cha UN kitakachokwenda DRC kupambana na waasi, kitajumuisha wanajeshi kutoka Tanzania, Malawi na Afrika Kusini.
Taarifa zinasema kuwa watu 19 wameuawa na wengine 27 kujeruhiwa katika mapigano kati ya waasi na wanajeshi wa serikali mjini Goma DRC.
Mapambano yalikuwa makali kwa siku ya pili huku katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon akitarajiwa kuwasili mjini humo hapo kesho, kama sehemu ya ziara yake ya eneo hilo.

No comments: