Tuesday, December 18, 2012

Kikosi Yanga kuanikwa rasmi leo

Wachezaji wa timu ya Yanga wakiwa katika mazoezi ya ufukweni eneo la Coco Beach jana, kulia ni kocha wa timuhiyo.
Hatimaye kitendawili cha wachezaji gani watakaobaki, kuingia na kutoka ndani ya kikosi cha Yanga kitakachocheza mzunguko wa pili wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara kitateguka leo wakati uongozi wa klabu hiyo utakapotaja rasmi majina yote hadharani, imefahamika.

Kumekuwa na tetesi nyingi kuhusiana na wachezaji wa Yanga walioongezwa, kuachwa kabisa na pia kuhusiana na mahala watakapopelekwa walioachwa kwa mkopo, hali ambayo Katibu Mkuu wa klabu hiyo, Lawrance Mwalusako, amesema kuwa itafikia mwisho leo wakati watakapoanika kila kitu mbele ya waandishi wa habari kwenye makao makuu ya klabu hiyo, Jangwani jijini Dar es Salaam.

Mwalusako aliiambia NIPASHE jana kuwa orodha ya majina ya watakaitangaza rasmi leo .

imezingatia mapendekezo ya benchi la ufundi la timu yao linaloongozwa na kocha Mholanzi, Ernie Brandts na kwamba, wana matumaini makubwa ya kuendelea kufanya vizuri katika mzunguko wa pili.

“Timu yetu inaendelea vizuri na mazoezi ya kila siku na kesho (leo) tutataja wachezaji wetu ambao kocha amewapendekeza kwa ajili ya mzunguko wa pili,” alisema Mwalusako.

“Kuna mambo mengi sana yamekuwa yakisemwa kuhusu Yanga, lakini tulikuwa makini katika kuangalia wachezaji watakaotufaa ili tuendeleze ushindi na hatimaye kutwaa ubingwa wa msimu huu," aliongeza.

Yanga ambao ni mabingwa wa Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati (Kombve la Kagame), wanaongoza katika msimamo wa ligi hiyo wakiwa na pointi 29, pointi sita zaidi ya mahasimu wao wa jadi na mabingwa watetezi Simba walioko katika nafasi ya tatu.

Mzunguko wa pili wa ligi hiyo inayotoa wawakilishi wa Tanzania Bara katika michuano ya Afrika utaanza mwezi ujao.

 
CHANZO: NIPASHE

No comments: