Sunday, June 2, 2013

Mtikisiko Polisi, vigogo watarajiwa kustaafu


*********
Habari za uhakika kutoka ndani ya Jeshi hilo zimedokeza kuwa Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, Inspekta Jenerali Said Mwema anatarajiwa kustaafu mwezi ujao na haijafahamika kama ataongezewa mkataba ama la.
Vyanzo mbalimbali vimedai kuwa japokuwa IGP Mwema anasita kukubali kuongezewa muda, lakini Rais Jakaya Kikwete anaonelea aongezewe muda ili wamalize pamoja uongozi wao mwaka 2015.
IGP Mwema ambaye alikuwa Ofisi ya Polisi wa Kimataifa (Interpol) Jijini Nairobi, Kenya, aliteuliwa kushika wadhifa wake huo mwaka 2006 na Rais Kikwete, kumrithi Omar Mahita ambaye alistaafu.
Habari zinasema endapo IGP Mwema hatapewa mkataba wa ama miaka miwili, basi ni dhahiri Rais Kikwete atakuwa na kibarua kigumu cha kuanza mchakato wa kumtafuta mrithi wake.
IGP Mwema anachukuliwa kama mmoja wa viongozi wa juu wa Jeshi hilo aliyelifanyia mapinduzi makubwa aliposhika madaraka hayo, ikiwamo kuja na dhana ya ulinzi shirikishi ama Polisi Jamii.
Tayari mabadiliko hayo yameaanza kufanyika kwa Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kinondoni jijini Dar es Salaam, Charles Kenyela kuhamishiwa makao makuu ya jeshi hilo.
Taarifa zaidi zimepasha kuwa nafasi nyingine ya juu ambayo kuna dalili ya kuwepo kwa mabadiliko ni ya Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI), inayoshikiliwa na Robert Manumba.

Wanafunzi Bora wazungumzia matokeo

SAID JUMA IRANDO2
*****
Mwanafunzi bora wa kwanza kitaifa katika matokeo yaliyorekebishwa ya mtihani wa kidato cha nne uliofanyika mwaka 2012, Said Irando kutoka Shule ya Sekondari Feza ya jijini Dar es Salaam, ameeleza kushangazwa na matokeo hayo kwa kuwa hakuyatarajia.
Mwanafunzi huyo ambaye tayari ameshaanza masomo ya Kidato cha Tano katika Shule ya Sekondari Feza, alisema kuwa ingawa alisoma kwa bidii lakini hakudhani kama angeweza kushika nafasi ya kwanza kitaifa na kwamba anamini mafanikio yake kitaaluma yana ‘mkono wa Mungu’.
“Sikutegemea kabisa kuwa mwanafunzi bora, ingawa nilisoma kwa bidii kubwa nia yangu ilikuwa ni kutaka kufaulu tu; Ni Mungu amenisaidia,” alisema Irando.
Alisema kujituma katika masomo, mazingira mazuri ya kusomea na upatikanaji wa vifaa muhimu vya kujifunzia ndiyo yaliyomwezesha kusoma na kufanya vizuri.
Irando ambaye ni mtoto wa kwanza katika familia yenye watoto watatu, alisema kurekebishwa kwa matokeo ya kidato cha nne kulibadilisha alama za matokeo yake kutoka Daraja la kwanza akiwa na alama tisa hadi saba, zilizomfanya kuwa mwanafunzi bora kitaifa na mwafunzi bora wa kwanza kati ya wavulana kumi bora pia kitaifa.
Mwanafunzi huyo alibainisha kuwa pamoja na wazazi wake kuwa ni wafanyabiashara, yeye anatamani kuwa mhandisi ingawa bado hajajua atakuwa mhandisi katika tasnia gani.
“Natamani sana kuwa mhandisi hiyo ndiyo ndoto yangu ingawa bado sijajua nitakuwa mhandisi wa sekta gani,” alisema Irando.

No comments: