Friday, April 26, 2013

Waandamana kuhusu Korosho Tanzania

Takriban nyumba 20 zimeteketezwa katika maandamano yaliyofanywa na wakulima wa Korosho pamoja na waandamanaji wengine Kusini mwa Tanzania.
Hii ni kwa mujibu wa mbunge mmoja wa eneo hilo.
Mbunge huyo, Faith Mitambo alisema kuwa majengo mawili nyumbani kwake mjini Liwale, yalichomwa na kuwa nyumba zingine mali ya baadhi ya wanachama wa chama tawala CCM ziliteketezwa.
Uharibifu huo ulianza baada ya wakulima kulipwa kiasi kidogo cha pesa ikilinganishwa na zile walizokuwa wamekubaliana kulipwa na serikali baada ya kuiuzia mazao yao mwaka jana.
Polisi zaidi wamepelekwa katika eneo hilo kuzuia ghasia zaidi.
Bi Mitambo, aliyekuwa mjini, Dodoma, wakati huo aliambia BBC kuwa alikuwa anazuru eneo bunge lake kudadisi hali ilivyo.
Alipokea habari kuwa waandamanaji waliokuwa wanajumuisha vijana , walianza kufanya fujo vijijini mnamo Jumanne asubuhi hadi walipofika mjini Liwale saa za jioni.
Mkaazi mmoja wa mji huo aliambia BBC kuwa mnamo Jumatano kulikuwa na hali ya wasiwasi mjini humo na kwamba polisi walikuwa wamewarushia gesi ya kutoa machozi wandamanaji ili kuwatawanya.
Maelfu ya wakulima wadogo wadogo wanaopanda Korosho nchini Tanzania na ambao huvuna mazao yao mwezi Oktoba, huyauza kwa mashirika mbali mbali kwa bei waliyokubaliana.
Mwandishi wa BBC mjini Dar es Salaam, Erick Nampesya anasema kuwa wakulima walikubaliana kulipwa shilingi 1,200 pesa za Tanzania kwa kila kilo ya korosho hizo.
Mwishoni mwa mwaka jana, wakulima walilipwa sehemu ya deni lao.
Lakini pale waakilishi kutoka kwa mashirika walipokwenda katika wilaya ya Liwale, kuwalipa sehemu ya mwisho ya deni lao, wakawa wamebadilisha makubaliano waliyokuwa wameafikiana.
Wakulima walilipwa nusu au chini ya nusu ya deni lililokuwa limesalia, baada ya kuambiwa kuwa bei ya Korosho ilikuwa imeshuka sana katika soko la kimataifa.
Wanasiasa wakuu ambao wakulima hao wanawalaumu kwa kukosa kuwasaidia ndio walikuwa wamewaelekezea ghadbabu zao
Wakulima wamekuwa wakilalamika kuhusu msukosuko wa bei za Korosho ambayo huathiriwa zaidi kulingana na msimu.

No comments: